Ujasiriamali una umuhimu wa hali ya juu kwa watu wa karne ya 21 kama ifuatavyo.
Kuongeza pato
Kutokana na kuongezeka kwa ushindani wa
masoko ya bidhaa au huduma fulani katika jamii mbali mbali; makampuni mengi yamekuwa
yakiwaajiri watumishi ambao ni wabunifu ili kupitia ubunifu wao katika kampuni
waweze kuongeza kipato. Makampuni ya simu za mikononi yamejua siri hii ndiyo
maana utasikia promosheni na matangazo mbalimbali yote yakiwa na lengo la
kuvuta hisia za wateja ili waweze kuongeza kipato cha kampuni.
Kubuni vitu
vipya .
Ulimwengu wa karne ya 21 unatamani vitu
vipya; wajasiramali wanayo ari ya kuwa tofauti na hii inawasaidia sana kubuni
vitu vipya kila kunapokucha au kila baada ya Muda fulani.
Kutoa ajira
Mwalimu wa ujasiriamali akiwa anaongea na wanafunzi wake darasani
aliwahi kuwaambia kuwa Mjasiriamali hatafuti ajira ila anatengeneza ajira.
Binafsi nilipotafakari kauli yake nikakubaliana nayo kwani ubunifu wowote ni
muhimu akiyebuni aufikishe kwenye kilele na
kwa kuwa atahitaji msaada kwa vyovyote atakuwa amejiajiri na kuwaajiri
wengine.
Kupunguza umaskini
Kaka Omari alifika katika mji fulani akiwa
hana fedha hata kidogo akawa analalia mabox usiku kama godoro huku akifanya vibarua vya kubahatisha na akagundua kuwa
katika mji ule mzima hakuna mtu anayechoma mahindi; baada ya kupata kipato
kidogo cha 10,000 aliamua kwenda kununua mahindi mabichi 50 kila moja kwa
shilingi 100 sawa na shilingi 5000; debe la mkaa wa shilingi 3000; nauli yake
na mzigo 2000. Jioni ilipofika alichukua mawe matatu akawasha moto kwenye mafiga kwani hakuwa na jiko; kwa
sababu watu walikuwepo wengi eneo hilo, wakati alipoanza kumenya mahindi watu
walianza kuyasubiria yaive na kwa jioni hiyo aliuza mahindi yote 50 kila mhindi kwa bei ya shilingi 500 sawa na 25,000/= kesho yake aliendelea na biashara yake hiyo akaongeza
akanunua mahindi 100 na alipokuja kuyauza kila moja 500 akapata 50,000/=; Huyu
Omari amekuwa kila jioni anatenga 25,000 kama akiba; kipato chake kwa mwezi
kitakuwa 25,000x30=750,000/=; Kwa sasa Omari ana zaidi ya miaka mitano katika
mji huo na amekuwa maarufu na kwa sasa amejenga, ameoa na anatunza familia yake bila majuto pamoja
na biashara yake. Ujasiriamali hupunguza au kufukuza umaskini kabisa.
Kupunguza Uhalifu
Baada ya biashara ya boda boda kushika kasi
hapa nchini Tanzania; Rafiki yangu alipata nafasi ya kuongea na baadhi ya
madreva wa boda boda kwenye mji
fulani hapa nchini ambao awali walikuwa siyo watu waaminifu kutokana
na tabia waliyokuwa nayo kama vile kufanya fujo mitaani; katika mazungumzo yao walipokuwa
wanaongea walikiri kuwa biashara yao imewakosesha muda wa kuzurura mitaani bila
lengo na kusababisha maasi. Kauli kama hizi ni Ushahidi tosha kuwa Ujasiriamali
unapunguza uasi.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni